Lebo

07/08/2015

KUTUBU

Sehemu ya 3

 

Ungamo lile lililazimishwa kutoka katika moyo wake wenye hatia kutokana na hisia ya lawama ya kuogofya sana iliyokuwa ndani yake na kutazamia hukumu iliyokuwa mbele yake. Matokeo ambayo yangempata yalimjaza hofu kuu, lakini moyoni mwake haikuwamo huzuni yenye kina, yenye kuuvunja-vunja moyo wake, na kumwonyesha kwamba ni yeye aliyekuwa amemsaliti Mwana wa Mungu asiye na mawaa, na kumkana yule Mtakatifu wa Israeli.

Farao, alipoteswa kwa hukumu za Mungu, alikiri dhambi yake ili apate kuepuka adhabu zaidi; lakini mapigo yalipokoma, alizidi kufanya kiburi dhidi ya Mbingu. Watu hao wote waliomboleza kutokana na matokeo ya dhambi, lakini hawakuhuzunika kwa ajili ya dhambi ile yenyewe.

Lakini moyo unapoutii mvuto wa Roho wa Mungu, ndipo dhamiri yake itakapoamshwa, na mwenye dhambi atatambua kiasi fulani jinsi Sheria ya Mungu ilivyo kuu na takatifu, ambayo ni msingi wa utawala wake mbinguni na duniani. Yule “Nuru halisi, amtiaye nuru kila mtu ajaye katika ulimwengu” Yoh. 1:9, huvimulika vyumba vya siri vilivyomo moyoni, na mambo ya giza yaliyofichwa humo hufunuliwa. Kuhakikishiwa dhambi huyagusa mawazo na moyo.

 Mwenye dhambi anaitambua haki ya Yehova, na kujisikia ya kwamba anayo hofu kuu kuonekana, akiwa katika hatia na uchafu wake, mbele za yule Aichunguzaye mioyo. Anauona upendo wa Mungu, uzuri wa utakatifu, furaha ya kuwa safi; anatamani sana kutakaswa, na kurejeshwa katika ushirika na Mbingu.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Tuandikie maoni yako hapa. Leave your comments here