Lebo

27/09/2016

KAZI NA MAISHA ..............

SOMO LA PILI


Tukijitahidi hivyo kusaidia wengine, sisi pia tutabarikiwa. Hili lilikuwa ndilo kusudi la Mungu alipotupa sisi sehemu ya kufanya katika mpango wake wa ukombozi. Amewapa wanadamu fursa ya kuwa washirika wa tabia ya uungu, nao, kwa upande wao, wanapaswa kuitawanya mibaraka hiyo kwa wanadamu wenzao. Hiyo ni heshima ya juu kabisa, hiyo ni furaha ipitayo zote, ambayo inawezekana kwa Mungu kuwapa wanadamu. Wale wanaoshiriki hivyo katika kazi hiyo ya upendo wanaletwa karibu sana na Muumbaji wao.
Mungu angaliweza kuwapa malaika wa mbinguni ujumbe wa Injili, pamoja na kazi yote ya kutoa huduma ya upendo kwa wanadamu. Angaliweza kuzitumia njia nyingine katika kulitimiza kusudi lake. Lakini katika upendo wake usio na kikomo alichagua kutufanya sisi kuwa watenda kazi pamoja naye, yaani, pamoja na Kristo na malaika zake, ili tupate kushiriki katika mbaraka na furaha hiyo, na kutiwa moyo kiroho, mambo ambayo ni matokeo ya huduma hiyo isiyo na ubinafsi. Tunakuwa na moyo ule ule wa huruma aliokuwa nao Kristo tunaposhiriki mateso yake. Kila tendo la kujinyima kwa manufaa ya wengine huimarisha roho ya ukarimu katika moyo wa mtoaji, na kumfanya afungamane kwa karibu zaidi na Mkombozi wa ulimwengu, ambaye “alikuwa tajiri, lakini kwa ajili yenu akawa maskini, ili kwamba ninyi mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake.” 2 Kor. 8:9, Na ni wakati ule tu tunapolitimiza kusudi la Mungu la kutuumba sisi, ndipo maisha yanaweza kuwa mbaraka kwetu.

Endapo utafanya kazi kama Kristo alivyokusudia wafuasi wake wafanye, na kuongoa roho za watu kwa ajili yake, utaona haja ya kuwa na uzoefu wa maisha wenye kina zaidi na ujuzi mkubwa zaidi katika mambo ya Mungu, tena utaona njaa na kiu ya kuitafuta haki yake. Utamsihi sana Mungu, na imani yako itaimarishwa, na nafsi yako itakunywa maji mengi katika kisima cha wokovu. Kupambana na upinzani na maonjo kutakufanya uikimbilie Biblia na maombi. Utakua katika neema na katika kumjua Kristo, nawe utakuwa na uzoefu wa thamani.
Roho ya kuwatumikia wengine bila ya kuwa na ubinafsi inaifanya tabia iwe na kina, thabiti, tena iwe na upendo wa Kristo, inaleta amani na furaha kwa yule aliye nayo. Hamu ya kupata mambo yaliyo bora huongezeka. Hakuna nafasi kwa uvivu, wala uchoyo. Wale wanaojizoeza hivyo kutumia hisani zao za Kikristo watakua kiroho, tena watakuwa na nguvu katika kufanya kazi ya Mungu. Watakuwa na utambuzi safi wa kiroho, na imani thabiti inayozidi kukua, na uwezo ulioongezeka katika maombi yao. Roho wa Mungu, anapoigusa mioyo yao, anataka pawe na amani takatifu moyoni, kama
jibu la mguso huo wa Mungu. Wale wanaoutumia muda wao wote kutenda kazi hiyo bila
ya kuwa na ubinafsi kwa ajili ya manufaa ya wengine wanafanya kazi ya kuziokoa roho zao wenyewe kwa hakika kabisa.

Njia pekee ya kukua katika neema ni ile ya kufanya kazi ile ile aliyotuagiza Kristo kuifanya  pasipo kujifikiria wenyewe, kwa uwezo wetu wote, kuwasaidia na kuwaletea furaha wale wanaohitaji msaada wetu tuwezao kuwapa. Nguvu zinakuja kwa kufanya mazoezi; kujishughulisha ndilo sharti hasa la kuwa na uzima. Wale wanaojitahidi kudumisha maisha yao ya Kikristo kwa kupokea mibaraka inayowajia kwa njia ya neema pasipo kujishughulisha, wala kufanya kazi yo yote kwa ajili ya Kristo, wanajaribu tu kuishi kwa kuendelea kula bila kufanya kazi. Na katika ulimwengu wa
kiroho kama ilivyo katika ulimwengu wa asili, matokeo yake sikuzote ni uharibifu na
uozo. Mtu ambaye angekataa kufanya mazoezi ya viungo vyake angepoteza uwezo wote wa kuvitumia baada ya muda mfupi. Hivyo Mkristo ambaye hazitumii nguvu zake alizopewa na Mungu siyo tu kwamba anashindwa kukua katika Kristo, bali anapoteza
nguvu alizokuwa nazo tayari.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Tuandikie maoni yako hapa. Leave your comments here