Hapo ndipo wengi wanapopotea, na hivyo hushindwa kupokea msaada anaotaka kuwapa Kristo. Wao wanadhani kwamba hawawezi kuja kwa Kristo isipokuwa kwanza wawe wamekwisha kutubia
dhambi zao, na ya kwamba kutubu kunawaandaa kupokea msamaha kwa ajili ya dhambi zao. Ni kweli kwamba kutubu kunakuja kabla ya msamaha wa dhambi; maana ni moyo ule tu uliovunjika na kupondeka, unaoona kwamba unamhitaji Mwokozi. Lakini je! ni lazima mwenye dhambi angoje mpaka amekwisha tubu kabla ya kwenda kwa Yesu? Je! toba iwe kizuizi kati ya mwenye dhambi na Mwokozi?
Katika Biblia, yaani, Neno la Mungu, hatusomi kwamba mwenye dhambi hana budi kutubu kabla ya kukubali mwito wa Kristo asemaye, “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha.” Mt. 11:28. Ni uwezo unaotoka kwa Kristo unaowawezesha watu kutubu kweli kweli. Petro aliwaeleza Waisraeli mambo haya kwa dhahiri aliposema, “Mtu huyo Mungu amemtukuza kwa mkono wake wa kuume, awe Mkuu na Mwokozi, awape Waisraeli toba na msamaha wa dhambi.” Mdo. 5:31.
Kadiri tusivyoweza kusamehewa dhambi bila Kristo, ndivyo tusivyoweza kutubu pasipo Roho wa Kristo kuziamsha dhamiri zetu. Kristo ndiye asili ya kila fikara njema. Yeye tu ndiye awezaye kupanda mbegu ya kuchukia dhambi katika moyo. Kila tamaa moyoni mwetu ya kutaka kuijua kweli na kuwa na maisha safi, kila kusadikishwa moyoni mwetu kunakotuonyesha kuwa sisi ni wenye dhambi, ni ushahidi uonyeshao kwamba Roho Mtakatifu anafanya kazi mioyoni mwetu.