Lebo

29/11/2016

Kujifunza Kuomba Maombi ya Kweli

SEHEMU YA KWANZA



MUNGU huzungumza nasi kupitia katika viumbe vyake vya asili na mafunuo yake, kupitia katika maongozi yake, na kwa njia ya Roho wake. Lakini njia hizo hazitoshi; sisi pia tunahitaji kumfungulia mioyo yetu. Ili tupate uzima wa kiroho na nguvu yake, hatuna budi kuongea na Baba yetu aliye mbinguni. Mawazo yetu yanaweza kuvutwa kwake; tunaweza kuzitafakari kazi zake, rehema zake, baraka zake; lakini hayo, kwa maana yake kamili, si kuongea naye. Ili tuweze kuongea na Mungu, ni sharti tuwe na mambo fulani ya kumwambia hasa kuhusu maisha yetu tunayoishi.Katika kuomba tunamfunulia Mungu mioyo yetu na kuongea naye kama tunavyoongea na rafiki wa kweli. Si lazima kufanya hivyo ili kumjulisha Mungu hali yetu ilivyo, bali kuongea naye kunatuwezesha kumpokea mioyoni mwetu.

Maombi hayamlazimishi Mungu kushuka kwetu, bali ni sisi ambao tunainuliwa mpaka kufika
kwake. Yesu alipokuwapo hapa duniani, aliwafundisha wanafunzi wake kusali. Aliwaagiza waweke mahitaji yao ya kila siku mbele za Mungu, na kumtwika mizigo yao yote. Na ahadi ile aliyowapa kwamba dua zao zingesikilizwa ni ahadi iliyotolewa kwetu pia. Yesu mwenyewe, alipokaa na wanadamu, aliomba mara nyingi.
Mwokozi wetu alishiriki katika shida zetu na udhaifu wetu; hivyo akawa mhitaji na mwombaji, akimwomba Baba yake ili apate nguvu mpya za kufanya kazi yake na kuwa tayari kupambana na kazi na majaribu yatakayompata. Yeye ndiye mfano wetu katika mambo yote. Ni ndugu yetu ashirikiye udhaifu wetu, “alijaribiwa sawasawa na sisi katika mambo yote;” lakini kwa sababu alikuwa hana dhambi, aliyaepuka maovu nafsini mwake; alistahimili mapambano na maumivu makali moyoni mwake katika dunia hii yenye dhambi. Ubinadamu wake ulifanya maombi kuwa ya lazima kwake na haki yake.

Alipata faraja na furaha katika kuongea na Baba yake. Na iwapo Mwokozi huyo wa wanadamu, Mwana wa Mungu, aliona kwamba anahitaji kuomba, je! sisi, tulio wanadamu dhaifu wenye dhambi, tusingeona kwamba ni jambo la lazima zaidi kwetu kuomba bila kukoma. Baba yetu aliye mbinguni anangojea kutumwagia baraka zake juu yetu kwa utimilifu. Ni fursa yetu kunywa maji mengi kwenye chemchemi ya pendo lake.
Ni jambo la kushangaza jinsi gani ya kwamba sisi tunaomba kidogo mno! Mungu yu tayari, tena
anapenda kusikiliza maombi ya kweli ya mtoto wake aliye duni kabisa, walakini sisi kwa upande wetu hatuna moyo sana wa kumwambia Mungu haja zetu. Hivi malaika wa mbinguni wanafikirije kuhusu wanadamu maskini wasio na msaada wo wote, ambao wanakabiliwa na majaribu, wakati moyo wa Mungu uliojaa upendo usio na kikomo unapowaonea shauku nyingi sana, akiwa tayari kuwapa zaidi ya yale waombayo au kufikiria, na bado maombi yao ni kidogo sana, tena wana imani ndogo kabisa? Malaika wanapenda kusujudu mbele zake Mungu; wanapenda kuwa karibu naye. Wanaona kwamba maongezi yao na Mungu ni upeo wa furaha yao; lakini watoto wa dunia hii,
wanaohitaji msaada mwingi mno ambao ni Mungu pekee awezaye kuwapa, wanaonekana
kana kwamba wametosheka kutembea bila ya kuwa na nuru ya Roho wake, yaani, ushirika wa kuwako kwake.

Giza la Shetani huwafunika wale wanaoacha kuomba. Majaribu ya adui huyo anayonong’ona masikioni mwao huwashawishi wafanye dhambi; na hayo yote ni kwa sababu wao hawazitumii haki zote alizowapa Mungu katika mpango wa mbinguni wa maombi aliowawekea. Kwa nini wana na binti zake Mungu ni wazito sana kuomba, wakati maombi ni ufunguo katika mkono wa imani uifunguao ghala ya mbinguni, ambamo zimewekwa hazina za msaada na mibaraka isiyo na mwisho ya Mungu mwenye uweza wote? Tusipoomba bila kukoma na kukesha kwa bidii, tutakuwa katika hatari ya kutojali na kukengeuka kutoka katika njia ile ya haki. Adui hutafuta daima kuzuia njia iendayo kwenye kiti cha rehema, ili kwa maombi ya dhati na imani tusiweze kupokea
neema na nguvu ya kutusaidia kuyapinga majaribu.

KUMJUA MUNGU

SOMO LA TATU.



Tusifungue kabisa Biblia na kuyasoma maneno yake bila kuomba. Kabla ya kuzifungua kurasa zake ingetupasa kuomba ufahamu kutoka kwa Roho Mtakatifu, naye atatupa. Nathanaeli alipomwendea Yesu, Mwokozi alisema, “Tazama, Mwisraeli kweli kweli, hamna hila ndani yake.” Nathanaeli akamwambia, “Umepataje kunitambua?”Yesu akajibu, akamwambia, “Kabla Filipo hajakuita, ulipokuwapo chini ya mtini, nilikuona.” Yoh. 1:47,48. Na Yesu atatuona sisi mahali pa siri pa sala, ikiwa tutamwomba ili tupate kuelimishwa na kuyajua yaliyo ya kweli.

Malaika watokao kwenye ulimwengu ule wa nuru watakuwa pamoja na wale ambao kwa unyenyekevu wa moyo wanatafuta uongozi wa Mungu. Roho Mtakatifu humwinua na kumtukuza Mwokozi. Ni kazi yake kutuonyesha Kristo, na hali yake jinsi ilivyo yenye haki na usafi, na kutudhihirishia habari za wokovu mkuu tupatao kwake. Yesu alisema, “Atatwaa katika yaliyo yangu, na kuwapasha habari.” Yohana 16:14. Roho wa kweli ndiye mwalimu pekee awezaye kutujulisha
barabara ile kweli ya Mungu. Ni dhahiri kwamba Mungu huwaona wanadamu kuwa wa thamani kubwa, kwa kuwa alimtoa Mwanawe afe kwa ajili yao, tena amemweka Roho
wake kuwa mwalimu na kiongozi wa wanadamu daima.
               

Nataka nimjue Yesu,
Na nizidi kumfahamu;
Nijue pendo lake tu,
Wokovu wake kamili.

Nataka nione Yesu,
Na nizidi kusikia
Anenapo kitabuni,
Kujidhihirisha kwangu.

Nataka tena zaidi,
Daima kupambanua
Mapenzi yake, nifanye
Yale yanayompendeza.

Nataka nikae naye,
Kwa mazungumzo matamu.
Nizidi kuwaonyesha
Wengine wokovu wake.

Zaidi, zaidi,
Nimfahamu Yesu,
Nijue upendo wake,
Wokovu wake kamili.

28/11/2016

KUMJUA MUNGU

SOMO LA PILI.
                                                             

Jambo kuu la ukombozi ni moja ambalo malaika wanatamani kulichungulia; litakuwa ndiyo sayansi na wimbo wa waliokombolewa milele hata milele. Je, si jambo lifaalo kufikiriwa sana na kuchunguzwa nasi katika siku hizi? Rehema isiyo na kikomo na upendo wa Yesu, kafara iliyotolewa kwa ajili yetu, mambo hayo hututaka sisi tuyatafakari kwa makini na kwa uzito wake.

Tungeongelea sana juu ya tabia ya Mpendwa Mkombozi na Mwombezi wetu. Tungetafakari sana juu ya utume wake yeye aliyekuja kuwaokoa watu wake kutoka katika dhambi zao. Tukitafakari hivyo juu ya mambo makuu ya mbinguni, imani yetu na upendo wetu vitakua na kuwa na nguvu nyingi zaidi, na maombi yetu yatazidi kukubalika na Mungu, kwa sababu yatakuwa yamechanganyika na imani na upendo kwa wingi zaidi. Yatatolewa kwa akili na kwa dhati. Na tunapowaza mambo matakatifu, imani yetu itaongezeka kwake, na upendo wetu pia, tena kwa ajili hiyo maombi yetu yatazidi kukubaliwa na Mungu. Kuwa na imani na

Yesu kutazidi kuongezeka daima, pamoja na uzoefu hai wa maisha ya kila siku unaoutegemea uweza wake wa “kuwaokoa kabisa wale wote wamjiao Mungu kwa yeye.” Waeb. 7:25. Na tunapotafakari juu ya ukamilifu alio nao Mwokozi, tutatamani kugeuzwa tabia zetu kabisa, na kufanywa upya kufanana naye katika usafi wake. Patakuwa na njaa na kiu ya roho ya kutaka kufanana naye yule tumpendaye sana. Kadiri tunavyozidi kumfikiria zaidi Kristo, ndivyo kadiri tutakavyozidi kuongea habari zake kwa wengine na kumwakilisha ulimwenguni.
Biblia haikuandikwa kwa ajili ya wataalamu wa Biblia peke yao; kinyume chake, ilitayarishwa kwa ajili ya watu wa kawaida. Kweli zile kuu ambazo ni za lazima kwa wokovu zimeelezwa waziwazi kama nuru ya adhuhuri; wala hakuna mtu ye yote awezaye kukosa kuzielewa na kupotea njia isipokuwa ni wale wanaofuata maoni yao wenyewe badala ya mapenzi ya Mungu yaliyofunuliwa wazi.

Tusikubali kupokea ushuhuda wa mtu ye yote juu ya kile Maandiko yafundishacho, ila tujifunze sisi wenyewe maneno hayo ya Mungu. Tukiwaruhusu wengine kufikiri mambo ya Biblia kwa niaba yetu, tutakuwa na nguvu kama ya kiwete na uwezo uliopungua sana nguvu yake. Nguvu bora za akili zetu zinaweza kudumaa mno kwa kukosa mazoezi ya kufikiri juu ya mambo makuu yanayofaa kutafakariwa kiasi cha kuweza kupoteza uwezo wake wa kuelewa maana zenye kina za Neno la Mungu.
Ubongo wetu utapanuka ukitumika kuchunguza uhusiano uliopo kati ya masomo ya Biblia, Maandiko yakilinganishwa na Maandiko, na mambo ya kiroho yakilinganishwa
na mambo ya kiroho.Hakuna njia nyingine iliyokusudiwa kuitia akili nguvu nyingi zaidi kama ile ya
kujifunza na kuyachunguza Maandiko. Hakuna kitabu kingine kilicho na uwezo mkubwa mno wa kuyakuza mawazo yetu, kuzipa nguvu fahamu za ubongo wetu, kama zilivyo hizo kweli pana, ziadilishazo, za Biblia. Kama wanadamu wangejifunza na kulichunguza Neno la Mungu kama inavyostahili, wangekuwa na maarifa mengi na tabia bora, na kuwa na kusudi thabiti ambalo katika nyakati hizi ni shida mno kuliona.
Lakini kuna manufaa kidogo tu yanayopatikana kwa kusoma Maandiko kwa haraka. Mmoja anaweza kuisoma Biblia yote, lakini bado ashindwe kutambua uzuri wake, wala kuelewa maana yake yenye kina iliyojificha. Kujifunza kifungu kimoja cha maneno mpaka maana yake imekuwa dhahiri, na uhusiano wake na mpango wa wokovu unaeleweka wazi, kuna manufaa mengi sana kuliko kuzisoma sura nyingi kwa juu juu tu bila ya kuwa na kusudi lo lote dhahiri wala kupata mafundisho yo yote yanayojenga.

Biblia yako iwe karibu nawe kila mara. Kila upatapo nafasi, isome; jifunze mafungu yake kwa moyo. Hata wakati utembeapo mitaani, waweza kusoma fungu fulani, na kwa njia hiyo kulikaza mawazoni mwako.Hatuwezi kupata hekima bila kujitahidi kwa dhati na kujifunza kwa moyo wa maombi. Baadhi ya sehemu za Maandiko maana yake imekuwa dhahiri kabisa; lakini kuna sehemu nyingine ambazo maana yake si rahisi kufahamika mara moja. Maandiko yanapaswa kulinganishwa na Maandiko mengine. Lazima pawe na utafiti wa makini na kutafakari kwa moyo wa maombi. Na kujifunza kama huko kutapata malipo maradufu. Kama vile mchimba madini anavyogundua mabamba ya mawe ya madini ya thamani yaliyojificha chini ya uso wa nchi, ndivyo yule anayestahimili kulichunguza Neno la Mungu, kama hazina iliyositirika, azionavyo kweli za thamani kuu mno, ambazo zimefichwa asiweze kuziona mtafutaji mzembe. Maneno hayo ya uvuvio, tukiyatafakari mioyoni mwetu, yatakuwa kama vijito vitiririkavyo kutoka katika chemchemi ya uzima.

03/10/2016

KUMJUA MUNGU

SOMO LA KWANZA.



Kwa njia nyingi Mungu anajaribu kutujulisha tabia yake, ili tupate kumjua na kushirikiana naye. Viumbe vya asili huongea na akili zetu pasipo kukoma. Moyo unaofunguliwa wazi utaguswa na upendo na utukufu wa Mungu kama unavyoonekana katika matendo yake na katika kazi za mikono yake. Sikio lisikilizalo laweza kusikia na kuelewa ujumbe wa Mungu kupitia katika vitu hivyo vya asili. Mashamba ya kijani kibichi, miti mirefu sana, chipukizi na maua, wingu lipitalo, mvua inyeshayo, kijito kibubujikacho, utukufu wa huko mbinguni, huongea na mioyo yetu, na kutualika sisi ili tufahamiane na yeye aliyeviumba hivyo vyote.
Mwokozi wetu aliyafungamanisha, pamoja na vitu hivyo vya asili, mafundisho yake ya thamani. Miti, ndege, maua ya mabondeni, vilima, maziwa, na mbingu zinazopendeza, pamoja na matukio na mazingira ya maisha yetu ya kila siku, yote yalifungamanishwa na maneno yake ya kweli, ili mafundisho yake yapate kukumbukwa kwa njia hiyo, hata katikati ya shughuli nyingi za maisha ya taabu ya mwanadamu.

Mungu angependa watoto wake wapendezwe na kazi zake, na kufurahia uzuri wa kawaida, uliofichika, ambao kwa huo ameipamba nyumba yetu ya kidunia. Yeye ni mpenzi wa vitu vizuri, na kupita hivyo vyote ambavyo kwa nje hupendeza na kuvutia, yeye anaipenda tabia nzuri; angependa sisi tukuze usafi wa maisha na kuwa na maisha ya kawaida tu, yaani tabia zilizofichika kama zile za maua.Kama tutasikiliza tu, basi, viumbe vilivyoumbwa na Mungu vitatufundisha mafundisho ya thamani juu ya utii na kumtegemea yeye. Kuanzia na nyota ambazo zinafuata njia zao zisizo na alama katika anga za juu na kizazi kwa kizazi zinafuata njia yao ziliyowekewa, mpaka chini kwenye atomu ndogo kabisa, viumbe vya asili huyatii mapenzi ya Muumbaji. Tena Mungu hukitunza na kukilisha kila kitu alichokiumba.
Yule anayeyashikilia malimwengu yasiyohesabika katika eneo kubwa sana, wakati uo huo anajali mahitaji ya shomoro mdogo wa kikahawia aimbaye wimbo wake mdogo pasipo hofu.Wanadamu wanapoondoka asubuhi kwenda kazini, na wakati waombapo; wakati wanapokwenda kulala usiku; na wakati wanapoamka asubuhi; tajiri anapofanya karamu katika jumba lake, au maskini anapowakusanya watoto wake kukizunguka chakula chao kidogo, kila mmoja huangaliwa kwa huruma na upendo na Baba yetu aliye mbinguni.Hakuna chozi limtokalo mtu ambalo Mungu halioni. Hakuna tabasamu yo yote asiyoiona. Kama tungesadiki hivyo kabisa, mahangaiko yote yasiyofaa yangeondolewa mioyoni mwetu. Maisha yetu yasingejazwa na kukata tamaa mno kama yalivyo sasa; kwa sababu kila kitu, kiwe kikubwa au kidogo, kingeachwa mikononi mwake Mungu,
ambaye hachanganyikiwi kuona ongezeko kubwa la masumbufu yetu, wala halemewi na mizigo yake. Hapo ndipo tungeweza kuifurahia amani mioyoni mwetu ambayo kwa wengi kwa muda mrefu imekuwa kitu kigeni.

Akili yako inapoufurahia uzuri uvutiao wa dunia hii, hebu fikiria ulimwengu ule ujao, ambao haujui kamwe waa la dhambi wala kifo; ambao ndani yake uso wa maumbile hautakuwa na kivuli cha laana tena. Hebu mawazo yako na yapige picha na kuyaona makao ya waliookolewa, kisha kumbuka kwamba yatakuwa na utukufu mwingi sana kuliko mawazo yako makali sana yawezavyo kuiona picha ile. Katika zawadi mbalimbali alizotupa katika maumbile tunaona tu nuru hafifu mno ya utukufu wake. Imeandikwa, “Mambo ambayo jicho halikuyaona wala sikio halikuyasikia, wala
hayakuingia katika moyo wa mwanadamu, mambo ambayo Mungu aliwaandalia
wampendao.” 1 Kor. 2:9.
Mtunga mashairi pamoja na mwanasayansi anayeshughulika na viumbe vya asili wanayo mambo mengi ya kusema juu ya maumbile, lakini ni Mkristo anayeufurahia uzuri wa dunia hii kwa shukrani kubwa mno, kwa sababu anatambua kazi ya mikono ya Baba yake, na kuuona upendo wake katika ua na kichaka na mti. Hakuna mtu ye yote awezaye kutambua kwa ukamilifu umuhimu wa kuwapo kilima na bonde, mto na bahari, ambaye havioni vitu hivyo kuwa ni ufunuo wa upendo wa Mungu alio nao kwa mwanadamu.

Mungu husema nasi katika matendo yake na uongozi wake, tena katika mvuto wa Roho wake mioyoni mwetu. Katika mambo yanayotokea kwetu, na katika mazingira yetu, katika mabadiliko yanayotokea kila siku pande zote, twaweza kupata mafundisho ya thamani, kama mioyo yetu imekuwa wazi kuyatambua mafundisho hayo. Mtunga Zaburi, akifuatilia matendo na uongozi wa Mungu, asema hivi, “Nchi imejaa fadhili za Bwana.” “Aliye na hekima na ayaangalie hayo, na wazitafakari fadhili za Bwana.” Zaburi 33:5; 107:43. Mungu husema nasi katika Neno lake. Humo imefunuliwa dhahiri sana tabia yake, jinsi anavyowatendea wanadamu, na kazi yake kubwa ya ukombozi. Humo zimesimuliwa habari za wazee wakuu na manabii na watakatifu wengine wa zamani. Walikuwa ni watu wenye “tabia moja na sisi.” Yakobo 5:17. Tunaona jinsi walivyopambana na mambo ya kukatisha tamaa kama yale tuliyo nayo sisi, jinsi walivyoanguka majaribuni kama sisi tulivyoanguka; hata hivyo walijitia moyo tena, wakashinda kwa neema ya Mungu; na sisi tukiwaangalia, tunatiwa moyo katika jitihada yetu ya kupata haki. Tunaposoma habari za mambo makuu waliyoyapitia katika maisha yao, habari za nuru na upendo na baraka waliyofurahiwa nayo, na habari za kazi waliyoifanya kwa neema ya Mungu, ndipo roho ile iliyowaongoza wao inawasha mwako mtakatifu na tamaa mioyoni mwetu, na kutupa hamu ya kufanana nao katika tabia – kuwa
kama wao katika kutembea na Mungu.
Yesu alisema hivi kuhusu Maandiko ya Agano la Kale - na je! si zaidi sana kwamba yale ya Jipya ni ya kweli - “hayo ndiyo yanayonishuhudia,” yaani, yanamshuhudia Mkombozi wetu, ambaye ndani yake matumaini yetu ya uzima wa milele yamewekwa. Yoh. 5:39. Naam, Biblia nzima inasimulia habari za Kristo. Tangu habari za mwanzo juu ya kuumbwa kwa ulimwengu, - kwa kuwa “pasipo yeye hakikufanyika chochote kilichofanyika,” Yoh. 1:3, mpaka ahadi ya mwisho, “Tazama, naja upesi,” Ufu. 22:12, twasoma juu ya matendo yake, tena twaisikiliza sauti yake. Kama unataka
kumjua Mwokozi, jifunze Maandiko Matakatifu. Ujaze moyo wako wote maneno ya Mungu. Hayo ndiyo maji ya uzima, yanakata kiu yako. Hayo ndiyo mkate wa uzima utokao mbinguni. Yesu asema, “Msipoula mwili wake Mwana wa Adamu na kuinywa damu yake, hamna uzima ndani yenu.” Akazidi kueleza maana yake hivi: “Maneno hayo niliyowaambia ni roho, tena ni uzima.” Yoh.
6:53,63. Miili yetu imejengwa kutokana na chakula tulacho na kinywaji tunywacho; na
kama ilivyo katika vitu vya asili, ndivyo ilivyo katika mambo ya kiroho: ni kile tunachokitafakari sana kitakachotupa afya na nguvu katika tabia yetu ya kiroho.

28/09/2016

KAZI NA MAISHA.................

SOMO LA TATU


Kanisa lake Kristo ni njia aliyoiweka Mungu kwa ajili ya wokovu wa wanadamu. Kazi yake ni kueneza Injili duniani kote. Na wajibu huo umewekwa juu ya Wakristo wote. Kila mmoja, kulingana na kiwango cha talanta yake na nafasi nzuri anayopewa, anapaswa kutimiza agizo hilo la Mwokozi. Upendo wa Kristo, uliofunuliwa kwetu, unatufanya sisi kuwa wadeni kwa wote wasiomjua. Mungu ametupa nuru, si kwa ajili yetu wenyewe, bali kwa ajili ya kuiangaza juu yao. Wafuasi wa Kristo kama wangeamka na kufanya wajibu wao, kungekuwako na watu elfu wa kuhubiri Injili mahali palipo na mhubiri mmoja tu sasa katika nchi za kipagani.
Na wale ambao wasingeweza kujiingiza wenyewe kufanya kazi hiyo bado wangeweza kuisaidia kwa kutoa fedha zao, kuiunga mkono, na kwa maombi yao. Tena pangekuwa na juhudi kubwa zaidi katika kazi ya kuongoa roho katika nchi za Kikristo. Hatuna haja ya kwenda katika nchi za kipagani au hata kuondoka na kwenda nje ya mduara mdogo wa nyumba zetu, kama kazi yetu ipo pale, ili kuweza kumtumikia Kristo. Tunaweza kufanya kazi hiyo katika mduara wa nyumbani mwetu, katika kanisa,
miongoni mwa wale tunaoshirikiana nao, na miongoni mwa wale tunaofanya nao kazi au
biashara.

Sehemu kubwa sana ya maisha ya Mwokozi wetu hapa duniani ilitumika kwa kufanya kazi ngumu katika kiwanda cha seremala kule Nazareti. Malaika wahudumuo waliandamana naye huyo Bwana wa uzima alipotembea pamoja na wakulima wadogo na vibarua, bila ya kutambulikana wala kupewa heshima. Kwa uaminifu alikuwa akitimiza utume wake alipokuwa akifanya kazi yake ile duni sawasawa na wakati ule alipowaponya wagonjwa au kutembea juu ya mawimbi ya Galilaya yenye kurushwa huku na huku kwa dhoruba. Kwa hiyo, katika kazi zetu duni kabisa na vyeo vyetu vya chini kabisa katika maisha yetu tunaweza kutembea na kufanya kazi pamoja na Yesu.
Mtume Paulo asema, “Kila mtu na akae katika hali iyo hiyo aliyoitwa mbele za Mungu.” 1 Kor. 7:24. Mfanya biashara anaweza kufanya kazi yake kwa namna ambavyo anaweza kumtukuza Mungu kwa uaminifu wake. Kama yeye ni mfuasi wa kweli wa Kristo, basi, ataonyesha dini yake katika kila kitu afanyacho, na kuwadhihirishia watu roho ya Kristo. Fundi mitambo anaweza kuwa mwakilishi mwenye bidii na mwaminifu wa yule aliyefanya kazi ya sulubu katika hali duni ya maisha kati ya
vilima vya Galilaya. Kila mtu anayelitaja jina lake Kristo angefanya kazi kwa namna ambayo wengine, wakiyaona matendo yake mema, wavutwe na wamtukuze Muumbaji na Mkombozi wao.

Wengi wametoa udhuru ili wasivitumie vipawa vyao katika kumtumikia Kristo kwa sababu wengine wanavyo vipawa bora sana na hali yao ni nzuri sana. Wazo limeenea kote kwamba ni wale tu walio na talanta za pekee ndio wanatakiwa kutumia uwezo wao katika kumtumikia Mungu. Imekuja kuelewekwa na wengi kwamba talanta zinatolewa kwa kundi fulani tu lililopendelewa, na kuwaacha wengine, ambao, kwa kweli, hawatakiwi kushiriki katika kazi hizo ngumu au katika thawabu zake. Lakini haijaelezwa hivyo katika mfano huu. Bwana wa nyumba alipowaita watumishi wake,
alimpa kazi “kila mtu kwa kadiri ya uwezo wake.” Mt. 25:15. Tukiwa na moyo wa upendo tunaweza kufanya kazi duni kabisa za maisha “kama kwa Bwana.” Kol. 3:23. Upendo wa Mungu ukiwamo moyoni, utaonekana katika maisha yetu. Harufu nzuri ya Kristo itatuzunguka pande zote, na mvuto wetu utawainua watu na kuwaletea furaha.
Haikupasi kungojea matukio makubwa au kutarajia kuwa na uwezo wa ajabu kabla hujaenda kufanya kazi ya Mungu. Huna haja ya kuwaza ulimwengu utakuonaje wewe. Kama maisha yako ya kila siku yanashuhudia usafi wa maisha yako na unyofu wa imani yako, na wengine wameamini kwamba unataka kuwanufaisha wao, basi, juhudi zako hazitapotea kamwe. Wafuasi wa Yesu walio duni na maskini kabisa wanaweza kuwa mbaraka kwa wengine. Huenda wao wasitambue kwamba wanafanya jema lo lote maalumu, lakini kwa mvuto wao usiotambulikana wanaweza kuanzisha mawimbi ya mibaraka yatakayozidi kupanuka na kuwa na kina kirefu, na matokeo yake yenye mibaraka huenda wasiweze kamwe kuyajua mpaka siku ile ya mwisho ya kupewa thawabu zao. Wao
hawajisikii au hawajui kwamba wanafanya kitu cho chote kikubwa. Hawatakiwi kujichosha wenyewe kwa kuingiwa na wasiwasi juu ya mafanikio. Wao wanapaswa tu kusonga mbele kimya kimya, wakifanya kwa uaminifu kazi ile ambayo Mungu amewapa kufanya, na maisha yao hayatakuwa bure. Roho zao zitakuwa zikikua zaidi na zaidi na kufanana na Kristo; wao ni watenda kazi pamoja na Kristo katika maisha haya, na kwa njia hiyo wanajitayarisha kwa kazi ile ya juu zaidi na furaha isiyokuwa na huzuni ya maisha yale yajayo.

27/09/2016

KAZI NA MAISHA ..............

SOMO LA PILI


Tukijitahidi hivyo kusaidia wengine, sisi pia tutabarikiwa. Hili lilikuwa ndilo kusudi la Mungu alipotupa sisi sehemu ya kufanya katika mpango wake wa ukombozi. Amewapa wanadamu fursa ya kuwa washirika wa tabia ya uungu, nao, kwa upande wao, wanapaswa kuitawanya mibaraka hiyo kwa wanadamu wenzao. Hiyo ni heshima ya juu kabisa, hiyo ni furaha ipitayo zote, ambayo inawezekana kwa Mungu kuwapa wanadamu. Wale wanaoshiriki hivyo katika kazi hiyo ya upendo wanaletwa karibu sana na Muumbaji wao.
Mungu angaliweza kuwapa malaika wa mbinguni ujumbe wa Injili, pamoja na kazi yote ya kutoa huduma ya upendo kwa wanadamu. Angaliweza kuzitumia njia nyingine katika kulitimiza kusudi lake. Lakini katika upendo wake usio na kikomo alichagua kutufanya sisi kuwa watenda kazi pamoja naye, yaani, pamoja na Kristo na malaika zake, ili tupate kushiriki katika mbaraka na furaha hiyo, na kutiwa moyo kiroho, mambo ambayo ni matokeo ya huduma hiyo isiyo na ubinafsi. Tunakuwa na moyo ule ule wa huruma aliokuwa nao Kristo tunaposhiriki mateso yake. Kila tendo la kujinyima kwa manufaa ya wengine huimarisha roho ya ukarimu katika moyo wa mtoaji, na kumfanya afungamane kwa karibu zaidi na Mkombozi wa ulimwengu, ambaye “alikuwa tajiri, lakini kwa ajili yenu akawa maskini, ili kwamba ninyi mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake.” 2 Kor. 8:9, Na ni wakati ule tu tunapolitimiza kusudi la Mungu la kutuumba sisi, ndipo maisha yanaweza kuwa mbaraka kwetu.

Endapo utafanya kazi kama Kristo alivyokusudia wafuasi wake wafanye, na kuongoa roho za watu kwa ajili yake, utaona haja ya kuwa na uzoefu wa maisha wenye kina zaidi na ujuzi mkubwa zaidi katika mambo ya Mungu, tena utaona njaa na kiu ya kuitafuta haki yake. Utamsihi sana Mungu, na imani yako itaimarishwa, na nafsi yako itakunywa maji mengi katika kisima cha wokovu. Kupambana na upinzani na maonjo kutakufanya uikimbilie Biblia na maombi. Utakua katika neema na katika kumjua Kristo, nawe utakuwa na uzoefu wa thamani.
Roho ya kuwatumikia wengine bila ya kuwa na ubinafsi inaifanya tabia iwe na kina, thabiti, tena iwe na upendo wa Kristo, inaleta amani na furaha kwa yule aliye nayo. Hamu ya kupata mambo yaliyo bora huongezeka. Hakuna nafasi kwa uvivu, wala uchoyo. Wale wanaojizoeza hivyo kutumia hisani zao za Kikristo watakua kiroho, tena watakuwa na nguvu katika kufanya kazi ya Mungu. Watakuwa na utambuzi safi wa kiroho, na imani thabiti inayozidi kukua, na uwezo ulioongezeka katika maombi yao. Roho wa Mungu, anapoigusa mioyo yao, anataka pawe na amani takatifu moyoni, kama
jibu la mguso huo wa Mungu. Wale wanaoutumia muda wao wote kutenda kazi hiyo bila
ya kuwa na ubinafsi kwa ajili ya manufaa ya wengine wanafanya kazi ya kuziokoa roho zao wenyewe kwa hakika kabisa.

Njia pekee ya kukua katika neema ni ile ya kufanya kazi ile ile aliyotuagiza Kristo kuifanya  pasipo kujifikiria wenyewe, kwa uwezo wetu wote, kuwasaidia na kuwaletea furaha wale wanaohitaji msaada wetu tuwezao kuwapa. Nguvu zinakuja kwa kufanya mazoezi; kujishughulisha ndilo sharti hasa la kuwa na uzima. Wale wanaojitahidi kudumisha maisha yao ya Kikristo kwa kupokea mibaraka inayowajia kwa njia ya neema pasipo kujishughulisha, wala kufanya kazi yo yote kwa ajili ya Kristo, wanajaribu tu kuishi kwa kuendelea kula bila kufanya kazi. Na katika ulimwengu wa
kiroho kama ilivyo katika ulimwengu wa asili, matokeo yake sikuzote ni uharibifu na
uozo. Mtu ambaye angekataa kufanya mazoezi ya viungo vyake angepoteza uwezo wote wa kuvitumia baada ya muda mfupi. Hivyo Mkristo ambaye hazitumii nguvu zake alizopewa na Mungu siyo tu kwamba anashindwa kukua katika Kristo, bali anapoteza
nguvu alizokuwa nazo tayari.

26/09/2016

KAZI NA MAISHA........

SOMO LA KWANZA


MUNGU ndiye asili ya uhai na mwanga na furaha kwa malimwengu yote. Kama mionzi ya nuru kutoka juani, kama vijito vya maji kutoka kwenye chemchemi hai, baraka zinamiminika kutoka kwake kwenda kwa viumbe vyake vyote. Na kila mahali ambapo uhai wa Mungu umo ndani ya mioyo ya wanadamu, utabubujika kuwa upendo na mbaraka kwa wengine.
Ilikuwa ni furaha ya Mwokozi wetu kuwainua na kuwakomboa wanadamu walioanguka dhambini. Kwa ajili hiyo hakuyahesabu maisha yake kuwa ni kitu cha thamani kwake, lakini “aliustahimili msalaba na kuidharau aibu.” Ebr. 12:2. Kwa ajili hiyo malaika wanashughulika daima katika kazi ya kuwaletea wengine furaha. Hiyo ndiyo furaha yao. Ile ambayo watu wale wajipendao binafsi wangeiona kuwa ni kazi ya kuwavunjia heshima, yaani, kuwahudumia wale walio na hali mbaya na ambao kwa kila hali ni duni kwa tabia na hadhi zao, ndiyo kazi waifanyayo malaika wasio na dhambi.Roho aliyo nayo Kristo ya upendo unaojitoa mhanga ndiyo roho iliyoenea kule mbinguni,
na ndiyo msingi hasa wa furaha kuu iliyoko kule. Hiyo ndiyo roho watakayokuwa nayo
wafuasi wake Kristo, ndiyo kazi watakayofanya.

Upendo wa Kristo ukiwamo moyoni, kama manukato yenye harufu nzuri, hauwezi kufichika. Mvuto wake mtakatifu utawagusa wote tunaokutana nao. Roho ya Kristo ikiwamo moyoni ni kama chemchemi jangwani, inayobubujika na kuwaburudisha wengi, na kuwafanya wale walio tayari kuangamia kutamani kunywa maji ya uzima. Kuwa na upendo kwa Yesu kutadhihirika kwa njia ya kuwa na tamaa ya kutenda kama alivyotenda yeye, kwa madhumuni ya kuwaletea furaha na kuwatia moyo wanadamu. Kutaleta upendo, upole, na huruma kwa viumbe vyote vya Baba yetu aliye mbinguni anayevitunza.
Maisha ya Mwokozi wetu alipokuwa hapa duniani hayakuwa maisha ya raha, wala ya kujishughulikia mwenyewe tu, lakini daima alijitahidi kufanya kazi kwa bidii, bila kuchoka kwa ajili ya wokovu wa wanadamu waliopotea. Tangu kuzaliwa kwake mpaka kusulibiwa kwake pale Kalwari, alifuata njia ya kujinyima, wala hakutaka aachiliwe asifanye kazi za sulubu, safari zenye kumletea maumivu, na shughuli kwa watu zinazochosha mno na kazi za kawaida. Alisema, “Kama vile Mwana wa Adamu asivyokuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi.”
Mathayo 20:28. Hilo lilikuwa ndilo lengo moja kuu la maisha yake. Mambo mengine yote yalichukua nafasi ya pili na kulisaidia lengo hilo. Kilikuwa ni chakula na kinywaji chake kufanya mapenzi ya Mungu na kuimaliza kazi yake (Yoh. 4:34). Nafsi na umimi havikuwa na nafasi katika kazi yake.

Kwa hiyo wale wanaoshiriki neema ya Kristo watakuwa tayari kujinyima sana, ili wengine aliowafia wapate karama hiyo. Watafanya kila wawezalo kuifanya dunia hii iwe mahali pazuri kwa ajili ya kukaa kwao hapa. Roho hii ni matokeo ya hakika ya kukua kiroho kwa mtu yule aliyeongoka kweli kweli. Mara tu anapokuja kwa Kristo, ndani yake hujitokeza shauku ya kuwajulisha wengine jinsi alivyomwona Yesu kuwa rafiki wa thamani sana kwake; kweli ile iokoayo na kutakasa haiwezi kufungiwa moyoni mwake. Kama tumevikwa haki ya Kristo, na kujazwa furaha ya Roho wake akaaye ndani yetu hatutaweza kunyamaza. Kama tumeonja na kuona kwamba Bwana ni mwema, tutakuwa na jambo fulani la kusimulia. Kama Filipo alivyomwona Mwokozi, tutawaalika wengine
kuja mbele yake. Tutajitahidi kuweka mbele yao mambo ya kuvutia pamoja na mambo yale ya kweli ya ulimwengu ule ujao ili waje kwa Kristo. Tutakuwa na shauku kubwa kuifuata njia ile aliyokwenda Yesu. Tutatamani kwa dhati sana kwamba wale watuzungukao waweze kumwona “Mwana-Kondoo wa Mungu, aichukuaye dhambi ya ulimwengu.” Yoh. 1:29